Thursday 22 January 2015

Facebook Yamuomboleza Omar Babu

Mazishi yanapoisha, hofu ya uchovuhumchochea mwana kutaka kuutua uzito wa huzuni aliyonayo ili kuiridiha hali yake ya kawaida. Aliyefiwa hupawa motisha na wenzake kwa kutomuuliza athari za kifo.
Teknohama imekuwa na mchango mkubwa katika makuzi na maenezi na maendeleo ya lugha ya Kiswahili. Imewawezesha wataalamu, wapenzi, walimu na wanafunzi wa lugha hii kubadilishana maoni na mawazo kwa urahisi na wepesi. Uvumbuzi wa mitandao ya kijamii umechangia mno kukiendeleza Kiswahili na kukivusha mipaka ya uswahilini.mojawapo ya mitandao hii ni Facebook. Tangu uvumbuzi wake mwaka 2004 kule Marekani, Facebook imejitokeza kuwa maarufu miongoni mwa maashiki hawa wa Kiswahili. Nafasi ya utafiti wa Facebook kukishughulikia Kiswahili imepanda sana ukilinganisha na mitandao mingine ya kijamii ambayo hutumiwa na watumiaji wengine duniani.
Waasisi wa Facebook walilenga kuwawezesha wanafunzi kuwasiliana na kutambuana kila mmoja. Mtandao huu ulianzishwa kwa ajili ya wanafunzi wa chuo kikuu cha Harvard, lakini baadaye ulipanuka hadi vyuo vingine vya maeneo ya Boston, Ivy League, na Stanford University. Hatua kwa hatua ulifunguliwa katika vyuo vikuu vingine, na hata kufikia kwa kila mtu umri wa miaka 13 na zaidi. Wanafunzi, waalimu na Wapenzi wa Kiswahili kwa jumla ambao wamechangamkia mtanzao huu wameweza kutumia huduma mbalimbali ambazo hutolewa nao kukipigisha Kiswahili hatua. Wameunda kurasa na vikundi mbalimbali vya kushughulikia masuala yanayohusu lugha hii. Vikundi ambavyo wameviunda ni pamoja na Umbuji na Ulimbwende wa Lugha ya Kiswahili, Ramani ya Fasihi, Ramani ya Kiswahili KBC Redio Taifa, Jamvi la Fasihi, Bahari ya Mashairi, Lahaja za Kiswahili, Darasa la Tafsiri, Kisima cha Mashairi, Ushairi-Nikosoe Nijenge, Ukumbe wa Waswahili na Utamaduni Wao, Ukumbi wa Mashairi na vingine vingi.
Wanachama wa vikundi hivi kwa juma moja sasa wamekuwa wakumuomboleza mshiriki mmaarufu na mkongwe zaidi kwenye kumbi hizi. Omari Babu Marjan alijitokeza kuwa na mchango mkubwa kwenye takribani vikundi hivi vyote.
Katika kumkumba marehemu kama aliyechangia mno kundini, mdhibiti wa ukumbi wa Umbuji na Ulimbwende wa Lugha ya Kiswahili wenye washiriki 21, 050 kwa sasa ametundika picha yake kama picha ya kikundi chenyewe. Kwenye ukumbi huu ndiko rambirambi nyingi zilikotumwa. Wapo waliotunga mashairi kuonesha kwamba mwendazake alikuwa mshairi maarufi aliyewalea na kuwaelekeza. Wamemmiminia sifa za ukarimu, upole, mwenye mlahaka mwema na nyinginezo nyingi. Kibwagizo cha rambirambi zenyewe ni kwamba mchango wako ulioenziwa na wengi utawapita huku akiliacha pengo kubwa ambalo ni vigumu kumpata atakayeliziba. Isitoshe ukumbi huu ndio ulitumika kwa kiasi kikubwa kuyatangaza mauko yake pamoja na mipango yote kuhusu mazishi.
Kumbi ambazo hushughulikia mashairi nazo zimejaa tahalili za kishairi kumuenzi mwalimu huyu. Maudhui ambayo yametawala tungo hizi ni kuhusu jinsi mwalimu Omar alivyokuwa msitari wa mbele katika kuwalea, kuwaelekeza na kuwahimiza watunzi chipukizi. Alichangia mashairi yasiyopungua mia mbili. Isitoshe alikuwa na mazoea ya kusasisha hali yake kila mara kishairi. Kupitia kwa masasisho yake wengi walijifunza kwamba katika fasni ya utunzi, heri kuanza kwa ubeti mmoja kasha chipukizi akaendelea kukua. Aliwahi kushiriki malumbano kadha, yakiwemo malumbano ya pete ambayo walishiriki na rafiki yake tangu chuo kikuu Hassan Morowa. Ingawa mwalimu alikuwa msomi, hakupenda kujinasibisha na tabaka la maulama. Isitoshe kila mara watu walivyomrejelea kama bingwa, alikanusha hili na kusema dama yeye mwanafunzi. Kwa mfano hapa ni chapisho lake kwenye kikundi kinachoitwa Jamvi la Fasihi Juni 17, 2012.
“Mimi si gwiji wa haya mambo. Nimechakura “maakaba” nikaangukiya tungo hizi tatu ambazo ni mfano wa ulumbi. Kwangu mimi ulumbi mzuri ni wa tungo sampuli hii maana zinajisimamia zenyewe. Ukisoma kila shairi kivyake linajisimamia wala mtu hahitaji shairi la pili kuelewa maana. Al- akh Rashid Bakuli alitunga tungo S’ENDEKEZE JINO BOVU na mimi nikafuatiliza MSI JITO KWITWA TONGO. Al-akh Abubakar Hassan Mwamboga akatunga YONDA LIKOSAPO BUNGO. Tungo zote hizo tatu hizo zinalingana vina na pia idadi ya beti. Msomaji ambaye ni makini atajuwa moja kwa moja kwamba hizo tungo zina uhusiano. Ulumbi mzuri ni huo wa kufumba bila kutajana. Nimeshasema mimi si bingwa na pengine kuna watu walio na rai tafauti. Tunapojibu tungo za watunzi wengine, tujitahidi kujibu kwa vina vyao ili kutiya ladha kwenye hayo malumbano. Tusilalamike kwamba hayo ni masharti magumu. Ikiwa mtu ni mtunzi, hayo anayaweza kama kucheza! Chembelecho Ustadh Ahmad Nassir Juma Bhalo, Malenga wa Mvita:
“Kusota si kusangaa, na kwenda si kusimama”. Kuna suala la maendeleo. Nadhani msanii bora ni huyo aliye na nia ya kujiendeleza zaidi. Kwa hivyo watunzi wa tungo za Kiswahili, tusione tumefika na kujipakazia ubingwa tusiokuwa nao. Hata mwalimu ni mwanafunzi.
Mwalimu aliwahi kushiriki mijadala kuhusu lugha ya Kiswahili ikiwemo kuhusu usuli wa Fumo Liyongo, Mashairi huru ikiwa ni ya Kiswahili au la, Kiswahili Sanifu kipo au hakipo, Ngeli ya neno maiti, Tafsiri ya neno Facebook na mijadala mingine kadha ambayo wanachama wengi waliifuatilia na kuchangamshwa na mawazo yake ambayo aliyajengwa kwa misingi thabiti. Wengi hupitia mijadala hiyo kila mara ili kujikumbusha maswala muhimu kuhusu lugha ya Kiswahili. Mjadala mwingineo aliwahi kuibua ambao ulikuza fani ya utunzi ni kuhusu uhuru wa mtunzi. Mjadala wenyewe umechapishwa kwenye jamvi la Fasihi Januari 30, 2012. Kwa mantiki hii tunaweza kusema kwamba Omar alishangia katika kukiweza Kiswahili Mtandaoni hivi kwamba yeyote anayesakura anaweza kunufaika. Amekipa Kiswahili pumzi mpya kupitia mchango wake wa mijadala pamoja na mashairi aliyoyatunga na kuyachapisha kumbini.
Kupitia vikundi hivi wengi wamejiongezea marafiki pamoja na kuwasilisha maoni yao kuhusu mada mbalimbali ambazo huibuliwa na wanachama. Omar aliwafaa wengi na kifo chake kimewapokonya mtaalamu wa kutegemewa.